Striker machachari asiyeisha vituko Malimi Busungu na kiungo mshambuliaji wa Lipuli FC ya
Iringa, Salum Machaku wametimuliwa kwenye kambi ya timu hiyo.
Hiyo,
ikiwa ni siku chache kabla ya mechi ya Ligi Kuu Bara dhidi ya Mwadui FC
itakayochezwa kwenye Uwanja wa Samora mkoani Iringa.
Busungu
alijiunga na Lipuli kwenye msimu huu akitokea Yanga baada ya mkataba
wake kumalizika huku Machaku aliyewahi kuichezea akiwa ni mmoja wa nyota
walioipandisha timu hiyo.
Taarifa zilizopatikana zimeeleza wachezaji hao wametimuliwa kutokana na nidhamu mbovu waliyoionyesha ndani ya timu.
Mtoa taarifa huyo alisema, kikubwa ni ulevi uliopindukia, kutolala kambini mara baada ya mechi za ligi kumalizika, hivyo katika kutengeneza nidhamu ya timu, uongozi umefikia maamuzi ya kuwatimua licha ya uwezo na uzoefu wao mkubwa waliokuwa nao.
Aliongeza
kuwa, uongozi huo umetangaza kutokuwa na wachezaji hao kwa hivi sasa na
tayari wameondolewa kambini kwa muda wa siku tano huku wachezaji
wengine wakiendelea na maandalizi ya mchezo dhidi ya Mwadui.
“Wamekuwa
wakifanya vitendo hivyo vya ulevi mara tu baada ya mechi ya ligi, sisi
viongozi tumeamua kuwa hatutakuwa na wachezaji hao katika kipindi hiki,”
alisema mtoa taarifa huyo.
Walipotafutwa
wachezaji wenyewe hawakuweza kupatikana hadi tunaingia mitamboni lakini
alipotafutwa kocha wa timu hiyo, Selemani Matola juu ya suala hilo
alisema kwa ufupi: “Hao wachezaji hawapo kambini kutokana na utovu wa
nidhamu, ukitaka kujua sababu zaidi watafute viongozi.”